23.3 C
Dar es Salaam
HomeKilimo BiasharaWaziri Kabudi: Kilosa iendelee kulinda amani, kuimarisha kilimo na ufugaji wa kisasa

Waziri Kabudi: Kilosa iendelee kulinda amani, kuimarisha kilimo na ufugaji wa kisasa

Na Mwandishi Wetu, Kilosa

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na Wenye Ulemavu, Prof. Palamagamba Kabudi, amewataka wananchi wa Jimbo la Kilosa kuendelea kudumisha amani, utulivu na mshikamano huku wakiepuka vitendo vya uhalifu vinavyohatarisha usalama wa jamii na kudhoofisha shughuli za uzalishaji.

Akizungumza Agosti 5, 2026 katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Magomeni, Wilaya ya Kilosa, Prof. Kabudi alisema Serikali imejipanga kuboresha sekta ya mifugo kwa kuhamasisha ufugaji wa kisasa badala ya mfumo wa kuchunga mifugo kihamahama.

Amesema tayari eneo la Madoto limetengwa kwa ajili ya kuanzisha shamba la majaribio la malisho, hatua inayolenga kuongeza tija katika ufugaji na kupunguza migogoro kati ya wakulima na wafugaji.

“Tunataka wafugaji watoke kwenye mfumo wa kuchunga na waingie kwenye mfumo wa kufuga kwa tija. Hii itaongeza uzalishaji na kuimarisha amani katika jamii,” amesema Prof. Kabudi.

Aidha, amesema Serikali imeweka mkakati wa kuufanya ukanda unaopitiwa na Reli ya Kisasa (SGR), kuanzia Lumuma–Kidete hadi Mkata, kuwa kitovu cha kilimo cha umwagiliaji kwa ajili ya biashara ili kuongeza uzalishaji na kuinua uchumi wa wananchi.

Prof. Kabudi pia alisema Serikali inaendelea na mchakato wa kutangaza mabonde ya Kisaki, Manyenyere, Mabana na Mbigiri kuwa maeneo maalumu ya uzalishaji wa mazao ya mbogamboga.

Amesisitiza kuwa mabonde hayo ni rasilimali muhimu kwa maendeleo ya taifa, hivyo yanapaswa kulindwa na kutumika kwa shughuli zilizokusudiwa.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Magomeni, Dkt. Sudi Salum, alisema migogoro kati ya wakulima na wafugaji bado ni changamoto inayohitaji ushirikiano wa wadau wote ili kudumisha amani na kuongeza uzalishaji.

Amebainisha kuwa baadhi ya vitendo vya kuingiza mifugo katika mashamba ya wakulima kwa makusudi vimekuwa vikichochea migogoro isiyo ya lazima.

Naye mkazi wa Kata ya Magomeni, Tausi Ally, aliiomba Serikali kuendelea kuimarisha ulinzi shirikishi ili kudhibiti vitendo vya uhalifu, ikiwemo unyang’anyi na mashambulizi, vinavyoweza kuhatarisha usalama wa wananchi na kuathiri shughuli za maendeleo.

Amesema mazingira salama yatawawezesha wananchi kuendelea na shughuli za uzalishaji kwa amani na kuchangia maendeleo ya Jimbo la Kilosa.

spot_img

latest articles

explore more

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here