22.5 C
Dar es Salaam
HomeMahojianoBodi ya Chai yahamasisha matumizi ya chai kwa manufaa ya afya

Bodi ya Chai yahamasisha matumizi ya chai kwa manufaa ya afya

Na Mwandishi Wetu, Dodoma

Bodi ya Chai Tanzania imewahamasisha Watanzania kujenga utamaduni wa kunywa chai inayozalishwa nchini, ikisema matumizi ya kinywaji hicho yana faida mbalimbali za kiafya na yanaweza pia kuchochea ukuaji wa sekta ya chai na uchumi wa taifa.

Akizungumza katika Maonesho ya Kitaifa ya Wakulima ‘Nanenane’ yanayoendelea jijini Dodoma, Afisa Mkuu wa Mipango na Uhamasishaji wa Bodi ya Chai Tanzania, Godlove Myinga, amesema chai ina virutubisho na kemikali asilia zinazosaidia kuimarisha afya ya mwili na kupunguza hatari ya magonjwa mbalimbali.

Amesema miongoni mwa faida za chai ni kusaidia kuondoa sumu mwilini, kuboresha afya ya figo, kupunguza hatari ya magonjwa ya moyo, kuimarisha afya ya kinywa na meno pamoja na kuupa mwili kemikali asilia za polyphenols zinazosaidia kuulinda dhidi ya magonjwa.

Myinga ameongeza kuwa matumizi ya chai pia husaidia kupunguza uchovu wa akili, kuleta utulivu na kuchangia ustawi wa jamii, hivyo wananchi wanapaswa kuifanya kuwa sehemu ya utamaduni wa matumizi ya vinywaji vya kila siku.

“Pamoja na faida hizo, matumizi ya chai nchini bado ni madogo, kwani takwimu zinaonesha watanzania wanatumia takribani asilimia 10 pekee ya chai inayozalishwa nchini na sehemu kubwa iliyobaki inauzwa katika masoko ya kimataifa kutokana na ubora wake,” amesema.

Alitoa wito kwa wananchi kuchangamkia fursa zilizopo katika mnyororo wa thamani wa zao la chai kwa kuwekeza katika uzalishaji, uchakataji, ufungashaji na biashara ya chai ndani na nje ya nchi.

Hata hivyo, Myinga amesema Bodi ya Chai inaendelea kutumia Maonesho ya Nanenane na majukwaa mengine kutoa elimu kwa wananchi kuhusu faida za matumizi ya chai pamoja na fursa za uwekezaji zinazopatikana katika sekta hiyo.

Aliwahimiza wananchi kutembelea banda la Bodi ya Chai katika maonesho hayo ili kujifunza zaidi kuhusu ubora wa chai ya Tanzania na mchango wake katika afya na maendeleo ya uchumi.

spot_img

latest articles

explore more

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here